Ushauri wa Kimaisha

Dada Dinah Habari za Kazi? Mimi ni mdada mwenye umri wa miaka 35 nina watoto wawili wenye baba tofauti. Wa kwanza ana miaka 16 na wa pili ana 12.


Hapo nyuma nilikuwa sipo vizuri kimaisha kwani nilikuwa sina kazi. Baada muda nikapata kazi Mkoani, nikafanya kama miaka miwili hivi.


Then nikapata kazi yenye maslahi zaidi ya kule kwa mwanzo Mkoa mwingine, ambako ndio nyumbani kwetu kabisa kwa wazazi wangu.

Nilipokuja kuripoti nikafikia nyumbani hadi hii leo, kwani toka nianze nina
kama miezi sita hivi.

Tangu watoto wamezaliwa wamekuwa hapa kwa wazazi hadi hivi leo hii kwani  wazazi wangu hawataki niwachukue
nikakae nao mwenyewe.


Kwa hiyo hadi hii leo wote tupo hapa nyumbani ila najipanga
kuhama.

Swali: kuna vitu viwili ,vinanichanganya nina kahela kangu nawaza je nifungue biashara au nirekebishe nyumba ya wazazi wangu?

Yaani najiuliza sipati jibu kwani nyumba nayo ni ya kizamani sana naomba unishauri dada Dinah nijiongezee kipato kwa kufungua biashara
au nianze na ukarabati wa nyumba yetu?

Yote ni muhimu kwani napenda wazazi wangu wakae kwenye nyumba nzuri, nianze kwanza kukarabati nyumba then biashara ifuate au?


Kumbuka hao watoto mimi ndio baba na ndio mama maana sijaolewa na umri umeenda. Ningependa ufiche email yangu. Asante.

**********


Dinah anasema: Habari ni njema, shukurani kwa ushirikiano.

Najua kuna hisia ya Hatia inakusukuma au kukufanya utake kuanza kukarabati nyumba ya wazazi wako kama shukurani!

Lakini kumbuka ilikuwa chaguo lao kuwachukua watoto, hukuwalazimisha au kuwaomba wakusaidie hivyo huna haja ya kurekebisha nyumba kwasababu ya kuhisi "guilt" na badala yake fanya kitu ambacho una uhakika kitazalisha Pesa ulizonazo.


Biashara itakuwezesha kurekebisha Nyumba yenu, kuwasaidia kujikimu na wakati huohuo kutakuwa na muendelezo wa kipato cha pili kuingia.


Lakini pia, unaweza kufanya yote kwa wakati mmoja, endelea kubaki hapo kwa wazazi ili senti za kulipia Nyumba ya kupanga (kutoka kwenye Mshahara wako) ndio uitumie kurekebisha Nyumba ya Wazazi wako taratibu(kila mwezi). Na hizo pesa za pembeni zikafanye Biashara unayotaka kuifanya.


Nina Imani kuwa maelezo haya yatakupa mwanga zaidi, nafurahi kuwa sehemu ya Maamuzi yako Muhimu ya Kimaisha.


Kila la kheri.
Mapendo tele kwako...

Comments