Nimesamehe vya kutosha, sasa simuamini tena

Shikamoo dada dinah, pole kwa kazi.
Dada  nahitaji ushauri wako
Nina mpenzi wangu nampenda sana na yeye anaonyesha kama ananijali.

Tangu tuanze mahusiano ni miaka mitatu sasa. Kipindi tunaanza mahusiano aliniambia hana mpenzi na mimi nikamuamini, ila baada ya Wiki kadhaa mwanamke mmoja akanipigia na kudai kuwa huyo niliyenaye ni mpenzi wake!


Nilimuuliza yule mwanaume kuhusu mwanamke yule lakini yeye alikataa ila mwisho wa siku akaadmit kama alikuwa na mahusiano naye ila hamtaki tena akaniomba msamahi basi nikamsamehe.

Mwaka jana nikakuta msg kwenye simu yake anachati na mdada na huyo dada kamtumia picha za uchi nilipomuuliza alidai huyo ni rafiki yake tu, nilimuelewa na kumsamehe.

Ila kama mwezi hivi hatukuwa kwenye mawasiliano mazuri yaani ni ugomvi tu bila sababu. Siku moja nikakuta tena msg anachat na mwanamke na anamahusiano naye nilipomuuliza akasema kweli alianzisha mahusiano naye kutokana na kutoelewana kwetu na akaomba msamah nikamsamehe.


Ila  dada dinah yaani simuamini tena na nahisi bado ana mahusiano na huyo mwanamke. Nampenda sana ila simuamini kabisa na kila nikifikiria aliyonifanyia nakosa hata hamu ya kula.


Dada dinah naomba ushauri wako je nifanyeje??? Nampenda sana ila tabia yake naona inanishinda.


*************

Dinah anasema: Marhabaa mrembo, shukurani kwa ushirikiano.

Mtu kakudanganya mwanzoni kabisa mwa uhusiano utamuamini vipi? Ile ilikuwa dalili ya kwanza kuwa jamaa ni Muongo.....ona sasa umesamehe mpaka kusamehe inapoteza maana eti!

Unahitaji kusamehe mara moja na msamehewa(Mkosaji) kubadilika na kuacha uchafu wake wa tabia....akirudia kosa unanawa Mikono, unaenda kutafuta furaha bila yeye!


Kutokana na maelezo yako ni wazi huyo bwana ni Malaya na ni muoga kuachwa hivyo akiishagundua kuwa mwanamke kajua tabia yake chafu na kuna hatari ya kuachwa....anaanzisha uhusiano mpya wakati bado yupo kwenye uhusiano mwingine uliopo "hati hati".

Sasa akiachwa kwenye uhusiano "hati-hati" anaendeleza ule uhusiano mpya hivyo hatokaa bila mpenzi.

Ndio maana alikuambia kuwa yule alikuwa mpenzi wake lakini hamtaki, hakisema SINA UHUSIANO NAE....."Simataki" ilikupa matumaini na uhakika kuwa wewe ndio unatakiwa na upo peke yako(Kisaikolojia).

Wewe huku unashindwa kula wakati yeye yupo sehemu amekumbatia mwanamke mwingine na anafurahi kama hakuna Kesho!! Bibie umeangushwa, inuka jifute vumbi na uanze kusonga mbele taratibu.

Umevumilia visivyovumilika kwa Miaka mitatu na ameshindwa kukuheshimu wala kukuthamini, haitaji uwepo wako kwenye maisha yake Machafu.


Achana nae, unastahili mwanaume mwema, muaminifu,mwenye mapenzi ya kweli na mwenye kuthamini utu wa mwanamke.

Kumpenda mtu sana sio kigezo wala sababu ya kuendelea kuishi na mwanaume mjinga-mjinga hasa ikiwa anaweka Maisha yako hatarini.

Utaumia, Utajiuliza kwanini? Utalia, Utajutia muda uliopoteza, Utachukia kisha Utakubali kuwa uhusiano haukufai na utasonga mbele kirahisi bila yeye.


Kila la kheri.
Mapendo tele kwako...

Comments