Mchumba Hanipendezeshi...

Shikamoo da Dinah.
Asante kwa kutuelimisha na mungu akubariki sana.

Da dinah naomba ushauri wako kwa hali na mali maana nipo njia panda. Mimi ni mwanamke 27yrs nipo kwenye mahusiano miaka 4 sasa na tumebarikiwa kuwa na mtoto mmoja.

Tunatarajia kufunga ndoa miezi mitatu ijayo na tunaishi pamoja. Tatizo langu ni kwamba mimi nina mpenzi binafsi sana yeye hanifikilii kabisa anajipenda yeye tu.

Mimi nimemaliza Chuo na sina kazi kwa sasa, kwa kipindi cha nyuma kidogo nikiwa mwanafunzi nilikuwa nikijishughulisha na vibiashara vyangu ambavyo vilinisaidia kufanya mambo mengi pamoja na kujiendeleza kielimu na maisha kwa ujumla.


Nilikuwa simwombi huyo mpenzi kitu chochote, lakini mimi kama mwanamke siku zote nimekuwa nikimtekelezea mpenzi wangu anachohitaji kutoka kwangu na kujaribu kuremba penzi letu.

Katika suala la kunipenda naona ananipenda na hawezi kukaa mbali nami hata akisafiri kikazi basi atajitahidi kutekeleza majukumu arudi kabla ya siku  alizotakiwa kukaa huko.

Mawasiliano ni mazuri akiwa hayupo nyumbani hawezi kupitisha masaa mawili bila kunipigia LAKINI akiwa nyumbani ndiyo tunawasiliana vizuri but kuna wakati ana majibu mabaya sana kiasi kwamba hunifanya nipoteze mapenzi kwake.


Nashindwa kumwelewa huyu mpenzi wangu, tangu tumekuwa wapenzi hanijali mimi kama mwanamke wake haninunulii nguo, hanipi pesa ya Saloon hanifanyii kitu chochote kinachonihusu mimi binafsi.

Mimi ni mwanamke ninaejipenda kweli kwa kipindi cha nyuma nilijimudu mwenyewe kama nilivyoeleza hapo mwanzo lakini niliacha kila kitu baada ya kuwa Mjamzito, maana niliumwa sana. Hata baada ya kujifungua afya yangu haikuwa stable mpaka sasa.


Nikimwambia baby naomba pesa nikanunue nguo hizi zimechoka, nguo navaa miaka mitatu hizo hizo out of fashion kama unavyojua sisi wanawake inatakiwa tuwe nadhifu!


Lakini nitaambiwa nitakupa basi inaishia hapo. Cha ajabu yeye binafsi anajipenda sana ni kawaida kununua vitu vyake binafsi kama nguo au viatu kila mwezi tena vya bei ghali laki ngapi huko na saa zingine ataniita dukani mzigo mpya umeingia nimchagulie vitu vizuri lakini mimi mpenzi wake hanifikilii hata siku moja!

Kipato sio tatizo ana huo uwezo nikimwambia ataniahidi tu itaishia hapo nasindwa kuelewa tatizo nini?


Da dinah kuna wakati nahisi hanipendi labda yupo na mimi kwa sababu anajua nitamsaidia kujenga family basi, natamani hata siku moja mpenzi wangu anipe zawadi lakini hakuna!

Mpaka kuna wakati anasema "najinunulia mimi tu ngoja mke wangu usijali nitakupendezesha tu subiri" hapo unakuta anapima nguo kaniona mie mnyonge.

Najisikia vibaya na nahisi kama hana mapenzi ya dhati kwangu sababu tofauti na hayo kuna mambo mengi anayostahili kunisaidia ktk future yangu ( kusaidiana) lakini hakuna kitu.

Mimi nimekuwa nikimpa support kwa kila kitu niwezavyo lakini mwenzangu hapana. Nahisi  sina furaha na nimemchoka sasa natamani hata niachane nae na vikao vya harusi ndio vimeanza naona kama ananitumia kujifurahisha tu.

Niliona aibu siku nimeenda nyumbani kwetu Mama yangu amechukua pesa zake akaenda kuninunulia nguo, pochi na viatu ananiambia mbona nimevaa vitu vya zamani nami ni mke wa mtu hivi they expect to see me shining nilishindwa kumweleza ukweli.

Naomba ushauri wako da dinah nipo taabani.

************


Dinah anasema: Marhabaa Mrembo, shukurani kwa Ushirikiano.


Sasa siku ya Ndoa utavaa nini Mrembo? Usijejikuta unavaa gauni lako la mwaka juzi ambalo haliendani na sherehe husika na yeye anawaka na Suti Mpya!

Kabla sijaingia ndani! Makubaliano yenu yalikuaje? Malezi? Uchumi? Mipango na je mlikubaliana kuzaa au ilikuwa "bahati mbaya"?

Kwasababu mtu huwezi tu kuacha shughuli zako/Elimu ili uzae wakati hujui utakaezaa nae atakuangalia au mtasaidiana vipi (kama ni Mchumba/Mume)?


Mambo ya kushika Mimba kiholela ukitegemea Mwenye Mtoto atakutunza bila mipango ya mbeleni ni Uzamani na husababisha matatizo makuu kwa mwanamke, moja ni kama hili ulilonalo wewe.

Huyu mtarajiwa(mume) sio mbinafsi, angekuwa mbinafsi asingekuwa akiijali familia yake kwa mawasiliano na kukatisha safari zake ili awahi kurudi Nyumbani.

Kwani nani huwa ananunua mahitaji muhimu ya hapo nyumbani? Je huwa Mpenzi wako anakupatia Senti za manunuzi ya kila Siku/Wiki.....je huwezi kuwa unabajeti na ku-save kwa ajili yako?!!

Nadhani ama ulimzoesha kwa kujifanyia kila kitu mwenyewe bila kumshirikisha(ile twende shopping na kununua vitu pamoja) pale uhusiano wenu ulipoanza na wewe ukiwa unajitegemea Kiuchumi.

Wengi wainachanga hii "kujitegemea kiuchumi"....mwanamke kujitegemea kiuchumi haina maana anachukua "jukumu la mwanaume" kwenye familia/uhusiano au Jamii!

Au Mbahili....maana kuna aina mbili za Wabahili....(1)-Hawataki kutumia pesa zao kabisa (2) wana-prefer kuzitumia kwa ajili yao kuliko wenzao.


Pamoja na kusema hivyo inaonyesha wazi uhusiano wenu unakosa Nguzo kuu mbili ambazo ni Mawasiliano(sio kupigiana simu na kujuliana hali) bali kuzungumza kama Wenza na Ushirikiano.

Wenza huzungumzia mengi kuhusu maisha yaliyopo na yale yajayo, kupanga Mipango....Mipango ikiwa ni pamoja na "shopping" ya chakula na Mavazi sio kujenga na kufanya miradi.

Wenza hushirikiana kwenye kila kitu bila kujali nani anaingiza Pesa na nani hana Kipato.


Kabla hujakubali kuzaa nae au kufanya mapenzi bila KUJIKINGA dhidi ya Mimba ulipaswa kuzungumzia na kukubaliana "future" yenu kama wapenzi.....mtafanya nini kuhusu malezi ya Mtoto ikiwa mtazaa?.....utakapojifungua hutorudi kwenye shughuli zako, je mtasaidiana vipi mpaka utakapo kuwa tayari kurudi "job"? N.k.

Hii ni 2000s sio 80s Mrembo, hakuna kuacha kazi inayokuingizia Kipato na kuchanua Miguu bila Kinga wakati hujui kilicho mbele!!

Sasa fanya hivi; Mkiwa mmekaa vizuri na hakikisha anakusikiliza, anza....Mpenzi (Tumuite Paul) Paul hivi unajua kabla sijakutana na wewe/sijazaa nilikuwa najipenda sana?!! Ningewa kama nilivyo hivi sasa walahi usingevutiwa na mimi na tusingekuwa pamoja!

Mwanamke nimechakaa mpaka najichukia....navaa nguo za Miaka 3 iliyopita lakini Mume wangu unag'aa mpaka napata aibu!

Kila nikiomba senti za Shopping, mwenzangu unanipa ahadi zisizotekelezwa.....sasa mpenzi kama hutaki kunipendezesha Mkeo basi naomba Mtaji ili nifanye Biashara na ikilipa nitakurudishia.

Pia inabidi tutafute Msaidizi (Nanny) au tumpeleke mtoto Chekechea maana sitokuwa na Muda wa Kumuangalia hapa Nyumani.


Msikilize atakujibu nini?.....akikupa ahadi! Demand muda maalum kwani hutaki kupoteza muda!


Akilalama kuwa mtoto bado ni Mdogo na anahitaji Mama zaidi ya Msaidizi (kama mtoto ni chini ya miaka 4) basi Jaribu kumuelewesha(wanaume wengine hawajui) na mkumkumbushe jukumu lake kama Mumeo na Baba bila kufoka wala hasira ila kuwa firm(serious)!

Wanaume wengine walilelewa ovyo, kwamba wao ni majina na Maumbile tu, lakini hawajui majukumu yao mpaka wakumbushwe au kushikwa mkono na kuelekezwa.

Suala la yeye kuwa na majibu ya hovyo ambayo yanakufanya upoteze "mapenzi" itakuwa ngumu kwangu kusema lolote kwani hukuwa wazi kwa kueleza Majibu yake hayo hutokana na maswali ya aina gani kutoka kwako?

Siku nyingine (baada ya hili la kurembwa kupita na kufanikiwa)....rudini kwenye Nguzo ya mawasiliano tena, na mzungumze kuhusu hilo.


Kila la kheri.
Mapendo tele kwako...

Comments