Mchumba ananichanganya...

Pole na kazi.
Naomba ushauri juu ya hili lililonitokea. Nina Mchumba na ninasoma nae Chuo kimoja, tumeshapanga mambo mengi lakini nimekuja kugundua amenisaliti kwa kutembea na mtu mwingine.


Nilipomuhoji alilia sana akanambia amepitiwa na muda huo akachukua simu na kumpigia yule Mvulana na kumwambia kwamba hataki mawasiliano nae tena.


Hilo halikuniridhisha, ilipofika asubuhi nikawaita marafiki zake na marafiki zangu na pia nikamwambia amuite yule Mvulana. Nilivyo muhoji yule Mvulana akasema hakuwahi kuwa nae kimahusiano na akakataa kabisa.

Mchumba wangu yeye anakubali ila anasema mbele yetu kwamba ananipenda Mimi na akahaidi kutorudia. Aliona hiyo haitoshi akabadili namba za simu na kila muda anaomba msamaha. Rafiki zetu walitushauri tusameheane ila niendelee kumchunguza.

Je, wewe unanishaurije?

**********


Dinah anasema: Ahsante, shukurani kwa ushirikiano.


Mmechumbiana kienyeji/kimjini-mjini au kwa kufuata taratibu zote za kutambulishana kwenye familia zenu, Umetoa Posa na kutoa sehemu ya Mahari?

Kama mmechumbiana kienyeji hakuna haja ya kuendelea kuwa nae, ikiwa upo nae hapo Pua na Mdomo (Chuoni) ameshindwa kuwa muaminifu kwenye penzi lenu sasa mkiwa mnafanya kazi sehemu mbali-mbali (Mikoa tofauti) si ndio ataolewa kabisa?!!

Kuna issue za kuhusisha marafiki lakini sio hii(mnajitia aibu tu). Kumuweka kati mwenzenu (yule kijana) na marafiki zenu inaogopesha....hata ingekuwa mie ningekana kwa Nguvu zote.

Kubadilisha namba sio kielelezo kuwa hana uhusiano na mwanaume aliekusaliti nae....kumpigia simu na kumuambia hataki mawasiliano nae haina maana anamaanisha kwa huyo kijana.

Kumbuka kuna wake/waume wanafanya affair wakijua kuwa wao ni "wezi" na wanafurahia kuwa wezi....hivyo huelewana na "muibiwa" na kukufanya Fala ili waendelee kuibana....sijui unanielewa?!!.

Umeelezea tukio zima lakini hakuna mahali umeweka wazi hisia zako juu ya Mchumba wako tangu hayo yote yatokee. Wewe kama wewe unajisikiaje? Unataka kufanya nini kuhusu uhusiano wenu.


Fuata Moyo wako lakini usisahau akili yako nyuma....Kila la kheri.
Mapendo tele kwako...

Comments