Kwanini Wajua Mapenzi huachwa?

Habari Da Dinah, Mimi ni Mwanamke mwenye umri wa kati wa Miaka 30, nimeolewa na nina watoto Wawili. Naishi Dar lakini kikabila ni Mnyamwezi.

Hivi kwanini Makungwi wengi wameachika ikiwa wao ni mabingwa wa mambo ya Ndoa?


************


Dinah anasema: Habari ni njema kabisa, nashukuru.

Kusema ukweli sijui(inabidi tuwatafute tuwaswalike) ila nitasema ninachodhania.

Kwenye suala la kuachika/acha/achwa haliegemei sana kwenye kuyajua mambo kitandani, kwani Ndoa au Mahusiano sio Ngono pekee.


Natambua kuwa Makungwi wengi wa "Kizazi Kipya" wanafunza mwanamke kuonyesha mapenzi na mavituzi ili asiachwe....na sio Maisha ya Ndoa, Uzazi n.k.


Nadhani "ukitaka usiachwe" ni "Brand" inayouza sana....kwasababu kila mtu hataki kuachwa au hataki Ndoa yake "ifeli" ndani ya miaka michache....wote wanataka Ndoa zao zidumu muda mrefu.


Lakini wanasahau kuwa umri mkubwa wa Ndoa au Uhusiano sio kielelezo cha furaha au mafanikio kwenye Ndoa husika.


Baadhi huendelea kubaki kwenye Ndoa kwa sababu nyingine na sio Mapenzi, wengine huendelea kubaki kwenye ndoa kwa vile wanadhani umri mfupi wa Ndoa zao ni aibu kwenye jamii n.k.


Ili Uhusiano au Ndoa iwe yenye furaha inahitaji Nguzo kuu 5 ambazo ni Maelewano/Makubaliano, Mawasiliano, Heshima, Uvumilivu na Ushirikiano....Mengine yote hujitokeza humo.


Nguzo moja kati ya hizo ikikosekana hakika Ndoa au Uhusiano utayumba. Sasa mmoja asipotoa Ushirikiano kwenye Mawasiliano ili kuwe na Maelewano, amani na furaha hutoweka.


Hata kama unayajua sana Mambo kitandani, huwezi kuendelea kuishi na mtu asiekupa ushirikiano, asie kuheshimu, kukupenda n.k.

Kama umejitahidi kufanya yote au mengi uliyofundwa kama mke lakini Mume haonyeshi kuelewa au kutaka kubadilika ili muendelee kufurahia Muungano wenu then ni bora kutoka Ndoani.

Hivyo nadhani hao Makungwi ndoa zao zimefeli kwa sababu nyingi tofauti lakini wapo ni kutokupata ushirikiano kutoka upande wa pili.

Kwasababu mwanamke kafundwa haina maana ndio awe mtekerezaji wa mahitaji yote muhimu kwenye Ndoa. Ndoa ni umoja, Ndoa ni Timu....ndoa ni kuwa tayari kujifunza na kubadilika inapobidi ili muendane.


Natumaini utaridhia majibu yangu....


Kila la kheri.
Mapendo tele kwako...

Comments

Anonymous said…
Dinna umeshauri vyema haswa! Watu wengi wanadhani ndoa ni kile kitendo cha ngono kitandani tu!
Kumbe tendo lile ni 1/4 ya misingi minne ya ndoa kama ulivyoeleza hapo juu.