Mpenzi kaacha wivu, karelax ile mbaya!

Dinah habari za kazi na pole sana. Mimi ni Mwanamke mwenye umri wa miaka 32 na Mume wangu anakaribia 42. Ndoa yetu imejaaliwa mtoto Mmoja wa Kiume mwenye umri wa Miaka 4.

Tangu urafiki, uchumba na ndoa mume wangu alikuwa ni mwenye wivu wa mapenzi, sio wa kufokeana na kugombana.

Nikitoka lazima apige simu kuangalia kama nipo salama, kama nipo na wenzangu alikuwa akitaka kuongea nao ili kuhakikisha kuwa kweli nipo nao kama nilivyomuaga.

Tulipokuwa pamoja alikuwa ananishika Mkono kama vile anaonyesha kuwa mimi ni wake na nilikuwa nafurahi sana na kujisikia napendwa, nalindwa na ananijali.

Kuanzia mwaka jana, Mume wangu kaongeza mazoea na mmoja wa marafiki zangu lakini kwa vile nawaamini wote sina mashaka nao.

Kinachonitia mashaka ni mume wangu kuacha kuonyesha wivu, yaani karelax mno hadi nahisi kama vile hanipendi tena.


Je ni utu uzima unamnyemelea au kuna zaidi? Naomba ushauri. Asante.


************


Dinah anasema: Ahsante na shukurani kwa ushirikiano.

Unapofundwa unaambiwa wazi kuwa usimuamini sana mumeo (kwa asilimia zote) na ukiona ana-relax, mtingishie kiberiti makusudi (mfanye apate Wivu).

Kutokana na hali ya maisha ilivyo sasa mie ninasema Usimuamini Mpenzi wako kwa asilimia zote iwe ni Mwanamke au Mwanaume.

Kuna baadhi ya watu wanadhani kumuamini mtu ni sifa za Mke/Mume mwema, na baadhi hufikiri kuwa ni hali ya kujiamini wao kama wao.

Utasikia, kwanini uwe na wivu bwana? Kwani huna "confidence" mbele ya wanawake/wanaume wengine?....kakuchagua wewe, relax!

Kwamba wewe uwe huna habari hata kama mwenza achelewe, ashikane na kucheka na watu wengine, akae mahali kazunguukwa na marafiki zako/zake Watanashati/Waarembo....kwavile tu unamuamini kuwa hawezi kufanya kitu "stupid" na wewe unajiamini.

Wanasahau kuwa mara zote watu huwa hawaterezi na watu wageni au kutoka mbali....hao hao kwenye mzunguuko wenu ndio rahisi kushawishika au kushawishi mwenza wako.

Pia wanasahau (au hawajui) kuwa Wivu ni hisia kama zilivyo hisia za mapenzi na kwamba zinategemeana/shirikiana....Bila mapenzi hakuna Wivu na bila Wivu hakuna mapenzi.

Mtu haitaji kwenda mbali kutereza (cheat) na haitaji siku nzima, sekunde chache tu zinatosha kujenga mazoea alafu tabia na baadae uhusiano wa nje ya ndoa/uhusiano wenu.

Yeye kutokuwa au kuonyesha wivu ni dalili kuwa mapenzi yake kwako yanaanza kubadilika na kuwa "heshima" bila yeye kujua.

Anaweza kusema anakupenda sana lakini kama ghafla tu haonyeshi hisia alizokuwa nazo awali ni wazi kuna kitu kinaendelea.


Labda na wee ume-relax, huonyeshi mapenzi kwake hivyo inampunguzia nguvu na kujihisi ni yeye tu ndio anaependa.

Inasemekana mwanaume akifikia umri wa miaka 40+ huanza kujihisi kama vile alivyokuwa na miaka 25. Anahitaji kuhakikishiwa na kuonyeshwa kuwa anapendwa, anahitaji attention n.k.

Wanawake huwa tunadhani kuwa wanaume hawahitaji hizo mambo, ukweli ni kuwa wanahitaji ila approach yao ni tofauti na sisi wanawake.


Isije kuwa Shoga yako ndio anatoa attention, anamsifia, anamhakikishia kuwa bado "wamo"....

Hebu anza kufanya uchunguzi wa karibu kuhusu uhusiano wa Mumeo na huyo rafiki yako ili ujue kinachoendelea. Hilo moja.

Pili, mapenzi ni ya wawili na yana Nguzo zake. Nguzo muhimu zinazokosekana kwenu (kwa mujibu wa maelezo yako) ni Mawasiliano na Ushirikiano.

Zungumzeni kama wapenzi na kila mmoja wenu aweke wazi hisia na hofu zake ili iwe rahisi kwenu wote kujirekebisha na kuongeza ishirikiano ili kusonga mbele mkifurahia ndoa yenu.

Tatu, Punguza ukaribu na huyo rafiki yako mwenye mazoea na mume na kamwe asiguse tena nyumbani kwenu.

Nne, Ongeza effort kwenye kuonyesha mapenzi, kujali na kumhakikishia mumeo kuwa unampenda.


Kila la kheri!
Mapendo tele kwako...

Comments

Anonymous said…
Dunia ya sasa ni bora kuwa peke yako na kufahamiana na watu bila kukutana kuliko kuwa na marafiki ambao kutwa wako nyumbani kwako na kuendekeza ushemeji usio na mpango.

Rose Mhando aliimba rafiki yake aliesali nae, kula pamoja ndio aliekuwa adui yake.